Kifungu cha 18

Kifungu cha kumi na nane Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali.

Katika kaya ya Muthithi, paliishi mwanamume mosi na ahali wake. Mwanamume huyo aliitwa Koga. Alizimbua riziki yak e kwa kuwatekea wakazi maji. Naye mkewe alichuuza maandazi na vitakataka vingine katika chete ya Muthithi. Licha ya pato lao dogo, waliishi kwa furaha na buraha. Ni bayana kuwa, binadamu hapati vyote wala hanyimwi vyote. Siku ayami zilipita kitambo waja hao wabarikiwe na mtoto. Ni miujiza ya Mola kuwa ndoa yao ilidumu katika kipindi hicho. Wavyele wa Koga walikuwa wemempa himizo na sindikizo amtaliki mkewe na kufunga pingu za maisha na mke mwingine. Mke ambaye angewazalia wajukuu. Koga naye hakuyumba, alisimama tisti. Yeye alizidi kumwomba Mola na kusubiri. Nalo la wahenga likatimia mcha Mungu si mtovu na subira huvuta heri!

“Washauri” wengi walikosa uso Susia alipopata mimba kisha akajifungua. Nia zaombovu ziligonga mwamba. Lakini watu ni ngamba hawakosi la kuamba. Ghafla walizusha uvumi mwingine. Ulikuwa uvumi usiokuwa na msingi wowote. Uvumi ulioongozwa na chuki na kijicho. Eti Susia alikuwa na macho ya nje na mtoto wao alikuwa mtoto haramu. Yote hayo hayakuwavunja moyo Susia na kipenda roho chake. Badala yake, hayo yaliimarisha mahaba yao. Ndoa yao ilinawiri na kushamiri. Kweli ndoa hufungwa mbinguni. Wadaku wale walisalimu amri. Walibwaga silaha. Waliona kazi yao ilikuwa sawa na kufumbatia maji iwapo si kujaribu kukimbizana na upepo. Naam, naye Mungu hamwachi binadamu wake. Kaba, mwanao Susia na Koga, aliinukia kuwa mtoto mwenye bidii, adabu na mwajibikaji. Shuleni akawa na kichwa chepesi. Matendo na maneno yake yakawa ni ya kupigiwa mfano.

Licha ya uhawinde wa wavyele wake, yeye alijifunga nira curriculumni. Aling’amua bayana kuwa ngazi ya kupandia na kuondoka katika lile lindi la umaskini ilikuwa ni elimu. Daraja la elimu aidha lingemvusha hadi ng’ambo ya pili, ng’ambo ya ufanisi. Alizidi kujifunga kibwebwe. Alielewa kuwa, mtaka cha mvunguni sharti ainame na papo kwa papo kamba hukata jiwe. Si ajabu basi katika mtihani wa darasa la nane, alipata maksi za juu sana. Nacho chanda chema huvishwa pete. Alipata mdhamini wa curriculum yake ya shule ya upili. Kamwe hakugeuka kuwa mgema ambaye anaposifiwa tembo hulitia maji. Aliongeza bidii zake maradufu. Vilevile, hakujigeuza kuwa punda ambaye fadhila zake ni mashuzi. La hasha! Alikuwa kijana mwenye shukrani sana kwa mdhamini wake. Nusu muongo baadaye, kijana Kaba alijiunga na chuo kikuu.

Huko chuoni, maisha yalikuwa tofauti sana. Vishawishi vya kila nui vilikuwa tumbi nzima. Mbwamwitu kwenye ngozi za kondoo walikuwa wengi. Hata hivyo yeye hakujigeuza kuwa maji yafuatayo mkondo. Alikuwa na mikakati yake imara. Ingawa waambao waliamba mwenye njaa hana miko, Kaba alisimama imara kama chuma cha pua licha ya telezi na utepetepe tele wa maisha. Aliyaepuka mambo ya anasa kama ukoma. Alielewa fika kuwa anasa hunasa nayo raha ikipita hugeuka na kuwa karaha. Alifuzu chuuo kikuu na kuajiriwa na shirika moja la kimataifa. Mbali na hayo aliendelea na curriculum na kupata shahada ya uzamili. Mshahara wake ukawa wa kutajika, nyumba ya fahari na gari la kukodolewa macho. Kumbe bidii hulipa na zito hufuatwa na jepesi!

Maelezo ya msamiati

  • siku ayami – siku nyingi
  • simama tisti – simama imara, kutoogopa
  • kichwa chepesi – kuwa na uwezo wa kuelewa mambo haraka
  • karaha – balaa, -enye kuudhi

1. Ni kweli kusema Koga na mkewe:  

  1.  Walikuwa matajiri wa mali.                  
  2.  Walikuwa maskini wasiokuwa na furaha.
  3.  Waliishi kwa furaha na utulivu.              
  4.   Walikuwa na watoto wengi.                          

2. Ni nani hasa waliomtaka Koga amwoe mke mwengine?    

  1.   Susia.      
  2.   Wakweze Koga.          
  3.   Mavyaa na bavyaa wa Susia  
  4.    Majirani

3. ... binadamu hapati vyote wala hanyimwi vyote... Ni nini maana ya kifungu hiki kulingana na taarifa?

  1.   Koga na mkewe walikosa mtoto lakini waliishi kwa furaha
  2.   Koga na mkewe walikosa furaha kwa kumkosa mtoto.  
  3.    Koga na mkewe walikosa furaha lakini wakampata mtoto.  
  4.    Koga na mkewe walikuwa na furaha licha ya kutopata utajiri.

4. Ni nini maana ya kubwaga silaha?    

  1.   Kukubali kushindwa.        
  2.   Kuanguka.        
  3.   Kushinda vitani.        
  4.   Kukasirika.

5. Ni zipi sifa za Kaba kwa mujibu wa makala haya.

  1. Maskini mzembe.    
  2. Kijana mwerevu, mwenye ari na uajibikaji.
  3. Kijana mwepesi na mwenye macho ya nje.  
  4. Kijana pweke.

6. Ni yapi yangemkwamua Kaba kutoka biwi la umaskini?

  1.    Elimu              
  2.    Ujanja                
  3.    Wepesi              
  4.    Wazazi

7. Kwa nini Kaba alimpata mdhamini?  

  1.  Hakuwa na wazazi.         
  2.  Hakuwa na pesa.       
  3.  Alikuwa amefeli.        
  4.  Wazazi hawangeweza kumlipia karo licha ya kufua dafu katika mthani.

8. Kamwe hakugeuka kuwa mgema ambaye anaposifiwa hulitia tembo maji. Mwandishi anakusudia nini?    

  1. Kaba alianza kutumia tembo.     
  2. Kaba alizidi kujibidiisha.       
  3. Kaba alianza uvivu.    
  4. Kaba alingiliwa na tabia ya maringo.

9. Ni nini maana ya kujifunga kibwebwe?

  1.  Kuwa na bidii.      
  2.  Kufungwa grezani.  
  3.  Kupongezwa.
  4.  Kupata msaada.

10. Ni methali ipi haifai kuyaelezea maisha ya Kaba?

  1.   Penye nia ipo njia.     
  2.   Akufaaye kwenye dhiki ndiye rafiki   
  3.   Dhamira ni dira.   
  4.    Uzuri wa kuyu ndani mabuu.