Kifungu cha 8

Kifungu cha nane: Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali yatakayofuatia

Tulikuwa tukila chajio chetu baada ya siku iliyokuwa na shughuli tele. Mkabala wetu palikuwa na runinga. Mtangazaji aliendelea kusoma taarifa ya habari. Picha ya mtangazaji iliondoka na kupisha picha ambazo zilisababisha hamu yetu ya kula itokomee ghafla: picha za wahasirwa wa njaa katika baadhi ya sehemu nchini. Zilikuwa ni picha za kuhuzunisha – vitoto vilivyokuwa vimebaki mifupa vikiganda mikononi mwa mama zao. Vilikuwa vikilia kutokana na njaa. Vingine vilionekana viking’ang’ania kunyonya maziwa ya nina zao. Vinyonye nini maskini vitoto? Mama zao pia walikuwa fremu za watu. Walikonda na kukondeana. Nzi nao walionekana wakitua na kupaa machoni, puani na vinywani mwa vitoto vile. Kwa sababu moja au nyingine mama wale hawakujali nzi wale.

Labda hawakuwa na nguvu za kuwafukuza nzi hao. Au labda hawakuwaona nzi wale. Picha zile zilituhuzunisha mno. Kwa mara nyingine tena, tukaona sababu zaidi za kumshukuru Mola kwa hali yetu. Ingawa kilalio chetu kilikuwa duni, tuliona kwamba, hali yetu ilikuwa bora zaidi ukilinganisha na maskini wahasiriwa wale wa njaa. Si eti hatukuwa na shukrani kwa Mungu. Isisahaulike kuwa hata siku mbili hapo awali, tulikuwa tumetumia ujira wote wa wiki hiyo moja kuchangia hazina ya kuwasaidia wahasiriwa wa njaa nchini. Tulikuwa tumenunua nafaka na kuzipeleka katika vituo vya kukusanyia misaada hiyo Hatukuona ugumu wowote wa kufanya hilo licha ya kuwa, kazi yetu katika machimbo ilikuwa ni ya kuvunja mgongo. Tulielewa kuwa wema hauozi na kumpa mwenzio si kutupa. Picha za wahasiriwa wale zilitugusa sana kiasi cha kuahidi kuchangia tena katika hazina ile.

Tuliona huo kama wajibu wetu sisi wazalendo kuwasaidia wananchi wenzetu. Lakini habari na picha zilizofuata katika runinga ile ile zilituacha katika hali ya hasira. Zilikuwa ni habari za “walanchi” waliotiwa mbaroni wakikiuza chakula kilichokuwa kimetolewa kuwasaidia wahasiriwa wa njaa. Habari hizo zilinifilisi maneno. Niliitumbulia macho runinga ile bila kujielewa. Waama, ibilisi wa mtu ni mtu, na kufa kufaana. Fahamu ziliponirejelea nilijipata nikiwauliza wenzangu maswali tele. Utu ulienda wapi? Mbona binadamu akapofushwa na tamaa kiasi cha kutomfikiria binadamu mwenzake?

Kitendo cha kuiba chakula cha msaada ili mtu ajitajirishe ni cha aibu kwa ubinadamu. La kuhuzunisha zaidi ni kuwa, hawakuiba ili wao wenyewe wasife njaa. La. Waliiba ili wajitajirishe. Tayari wao walikuwa na chakula cha kutosha. Bali hawakuona haya kuiba wajitajirishe. Huenda wakawa ni matajiri wa pesa.Lakini ukweli ni kuwa, wao ni fukara fukarike wa huruma, busara na neema. Wanastahili maombi zaidi ya adhabu nyingine ile. Mungu wasaidie. Waondolee upofu wa tamaa na ubinafsi.

4. Ni sahihi kusema:    

  1. Vitoto vile havikujali nzi    
  2. Vitoto vile viliridhika kwa kunyonya.      
  3. Vitoto vile viliadhirika kwa utapiamlo.    
  4. Vitoto vile vilikuwa na siha nzuri.  

5. Mwandishi na wenziwe walizimbua riziki kwa:  

  1. kuchimba mawe.       kubeba mizigo.      
  2. kutazama runinga.          
  3.  kutoa misaada.

6. Ni sahihi kusema kuwa, mwandishi na wenzake walikuwa:      

  1. wakwasi wa mali.                
  2. watu wenye mikono birika.            
  3. mabahili wakubwa.                        
  4. wenye mikono wazi.

7. Waliokiiba chakula cha misaada ni:    

  1.  wananchi wazalendo.              
  2.  walanchi wanafiki, wafisadi na wachoyo.        
  3.  walalaheri waliokuwa na njaa.          
  4.  walalahoi waliokuwa na njaa.

8. Fahamu ziliponirejelea inaonyesha kuwa:

  1. mhusika alikuwa amechanganyikiwa sana.    
  2. mhusika alikuwa amezirai.        
  3. mhusika alikuwa amesahau jambo.    
  4.  mhusika alikuwa mgonjwa.

Maelezo ya msamiati

  • chajio – chakula cha jioni,kilalio
  • fukara fukarike – maskini sana

1. Ni jambo lipi lililosababisha wahusika wakose hamu ya kula?

  1.  Picha za walioathiriwa na njaa.   
  2. Picha ya mtangazaji.     
  3. Hali ya njaa nchini.        
  4. Sauti ya mtangazaji.

2. Vitoto vilivyokuwa vimebaki mifupa, maana yake ni:  

  1. Vitoto vilivyokuwa vimekonda sana.    
  2. Vitoto vilivyokuwa vimebaki na mifupa. 
  3. Vitoto vilivyokuwa vikila mifupa kwa kukosa nyama.
  4. Vitoto vichanga vigonjwa.      

 3. Ni jambo lipi linaloashiria kuwa, vitoto vile vilikuwa vichafu?  

  1. Vilikuwa vimekonda sana.       
  2. Vilikuwa vimeganda mikononi mwa mama zao.  
  3. Vilikuwa vikilia.        
  4. Viliwavutia nzi.

9. Kulingana na kifungu, vipofu ni akina nani?

  1. Wakiibao chakula cha msaada.    
  2. Wakataao kutoa chakula cha msaada.          
  3. Wanaoathiriwa na njaa.                        
  4.  Wasio na chakula.

10. Ni methali ipi mwafaka zaidi kuelezea hulka ya mwandishi na wenziwe?        

  1. . Kutoa ni moyo usambe ni utajiri.    
  2.   Kuishi kwingi ni kuona mengi.    
  3.    Ibilisi wa mtu ni mtu.                  
  4.   Yote yang’aayo si dhahabu.