Kifungu cha 2

Kifungu cha pili: Soma kifungu hiki kisha jibu maswali yafuatayo.

Katika kijiji cha Pwera, alizaliwa mtoto msichana aliyeitwa Waridi. Waridi alikuwa mtoto wa kipekee katika aila yake, kwani nduguze wawili waliomfuata hakuna aliyetoka uzalioni akiwa hai. Kwa miaka mitatu, kivuli cha simanzi kiliandama aila ya Waridi. Mambo yaliharibika zaidi wavyele wake Waridi walipoanza kusumbuliwa na polepole kulemewa na maradhi ya kila nui.

Kweli hakuna msiba usiokuwa na mwenziwe. Hali yao ya siha ilizidi kuzorota na si ajabu miaka miwili baadaye, wote wawili walitangulia mbele ya haki. Waridi akaachwa mtoto yatima. Nyota ya Waridi ilionekana kung’aa wakati wa mazishi ya hayati wavyele wake. Shangaziye ambaye alikuwa amezamia lulu mjini alifika na kusema angemsaidia Waridi. Angemlea na kumkimu kwa mahitaji yote. Bela, shangaziye Waridi alisemekana kuwa na pesa tele.

Sifa za ukwasi wake zilikuwa zikifika kijijini mara kwa mara. Hata hivyo shughuli zake huko mjini zilibaki kitendawili kisichokuwa na jibu kwa wanakijiji. Licha ya utajiri wake, Bela hakuwajali wavyele wake. Si ajabu wengi walistaajabia ukarimu wake kwa Waridi. Lakini haidhuru, kila shetani ana mbuyu wake. Kule mjini maisha yalikuwa ya raha mustarehe. Waridi alifurahia kila hali. Vyakula vitamu, hamamu ya kuogea, kutazama runinga.

Hata hivyo alipotaja mambo ya kujiunga na shule alielezwa asubiri huku akikumbushwa kuwa subira huvuta heri. Polepole unyemi uliendelea kuisha. Waridi akaanza kuachiwa kazi za pale nyumbani Bela na wanawe walipoondoka asubuhi. Umri wake mdogo haukumwepushia mzigo mzito aliobebeshwa pale nyumbani. Maskini Waridi aligeuzwa kuwa mjakazi pale chengoni.

Kamba yake ya matumaini ya kuendeleana curriculum ilikatika ghafla jioni moja Bela alipomweleza kimasomaso kuwa hakuwa na pesa za kupoteza na mtoto yatima. Malipo ya Waridi yalikuwa ni nguo kuukuu zilizokuwa zimetumiwa na watoto wa Bela. Waridi alijutia sana uamuzi wake wa kumfuata shangaziye. Heri angebaki na nyanyaye huko mashambani. Ingawa nyanyaye pia alikuwa na yake, afadhali zimwi likujualo, halikuli likakumaliza. Kumbe alikuwa ametoka kufiwako na kwenda kuliwako nyama!

Hali ilipozidi, Waridi aliamua kutoroka pale. Kwa nyota ya jaha alianguka mikononi mwa msamaria mwema aliyewajulisha maafisa wa polisi. Waridi alirudishwa kwa nyanya naye shangaziye akachukuliwa hatua za kisheria. Maelezo ya msamiati nui – aina unyemi – upya unaofurahiwa kwa muda tu hamamu – bafu chengoni – nyumbani

  •  Kwa nini watu wengi walitia shaka msaada alioahidiwa Waridi na shangaziye?

a. Kazi ya shangaziye haikujulikana.

b. Shangaziye hakuwa akija sana pale mashambani.

c Shangaziye alikuwa amewapuuza wazazi wake.

d. Shangaziye alikuwa na pesa tele.

  •  Hakuna msiba usiokuwa na mwenziwe inamaanisha:

a. Kuugua kwa wavyele wa Waridi kulifuatwa na kifo chao.

b. Kufa kwa nduguze Waridi kulifuatwa na kuugua kwa wazazi wake.

c. Vifo vyo wazazi wake Waridi vilifuatwa na mateso dhidi ya Waridi.

d. Misiba hutokea pamoja.

  • Kwa nini mwanzoni Waridi hakuchukuliwa na nyanyaye?

a. Nyanya yake hakuwa na uwezo wa kumsaidia.

b. Nyanya yake hakuwa na nia wala mapenzi ya kumsaidia.

c. Waridi alikataa kukaa na nyanya yake.

d. Waridi alitaka kuishi mjini.

  •  Kamba yake ya matumaini ya kuendelea na curriculum ilikatika ghafla! Maana yake ni:

a. Alilikosa lile alilotumainia.

b. Alilolitumainia huenda asilipate.

c. Angelipata alilolitumainia.

d. Palikuwa na uwezekano wa kutopata alilolitumainia.

  •  “… zilibaki kitendawili kisichokuwa na jibu…” inamaanisha:

a. Wanakijiji walikuwa na fununu za shughuli za Bela huko mjini.

b. Wanakijiji hawakumjua Bela.

c. Shughuli za Bela mjini hazikujulikana na wanashamba.

d. Bela hakuwa na kazi wala bazi huko mjini.

  •  Ni sahihi kusema:

a. Waridi aligeuzwa mtumishi wa Bela.

b. Waridi alitumikia Bela na wanawe.

c. Waridi alilipwa huduma zake kwa haki.

d. Waridi alifurahia kukaa kwake mjini.

  • Kwa nini Bela alikataa kumwelimisha Waridi?

a. Bela hakuwa na pesa za kumwelimisha Waridi.

b. Bela hakuyathamini maisha ya Waridi.

c. Bela hakuwa na mfanyikazi pale nyumbani.

d. Waridi hakupendelea kusoma.

  •  Zimwi likujualo halikuli likakumaliza inamaanisha:

a. Waridi alionelea heri kuishi mashambani kuliko kuishi na Bela.

b. Waridi alionelea heri mateso ya nyanyaye kuliko yale ya shangaziye.

c. Waridi alijuta kuandamana na Bela.

d. Waridi alipendelea kuishi peke yake kuliko kuishi na shangaziye wala nyanyaye.

  •  Kwa nini Bela alichukuliwa hatua za kisheria?

a. Kwa kumchukua Waridi hadi mjini.

b. Kwa kumpata Waridi mavazi ya watoto wake.

c. Kwa kutomliwaza Waridi. d. Kwa kukiuka haki za mtoto Waridi.

  • Kichwa bora zaidi kwa taarifa hii ni :

a. Waridi mtoto yatima.

b. Mateso ya watoto.

c. Haki za Waridi zakiukwa.

d. Waridi na shangaziye.