Visawe

- Haya ni maneno yaliyo na maana sawa au yanayokaribiana sana kimaana | kwa maana. 

1. Mtu – mja, adinasi, mahuluku, insi, binadamu. 

Mtu [a-wa]: kiumbe anayetembea wima ambaye hutumia fikira zake kwa ustadi bainifu zaidi ya viumbe vyote. 

Mfano katika sentensi - Mtu huyo ni mwoga | watu hawa ni waoga. 

 

2. Rafiki – msena, mwandani, bui, muhibu, sahibu, somo, msiri, mwenzi. 

Rafiki [i-zi]: mtu anayeaminiana na kupendana namwingine.

Mfano katika sentensi :- 

a) Nilikula kwenye kafeteria na sahibu wangu.

b) Nyaiko na Nyambane ni rafiki. Kila mara, wao hupatikana pamoja.

 

3. Adui – hasimu.

Adui [a-wa]: mtu au kiumbe anayemfanyia mtu mwingine uovu.

Mfano katika sentensi: Paka na panya walifanyika hasimu.

 

4. Baba – abu

Baba [a-wa]: mzazi wa kiume. 

Mfano katika sentensi - Leo tulikutana na baba wa taifa (rais) kwenye ikulu.

 

5 Mama – nina

Mama [a-wa]: mzazi wa kike. 

Mfano katika sentensi:-

a) Mama yangu anapenda ukulima zaidi.

b) Kitinda mimba wetu anafanana na Mama.

 

6. Msichana – banati, gashi, binti, mwanamwali. 

Msichana [a-wa]: Kijana wa kike aliyebaleghe lakini bado hajaolewa au kuzaa.

Mfano katika sentensi: Msichana huyu anasomea uhandisi katika chuo kikuu cha Egerton.

 

7. Mvulana – mvuli, ghulamu

Mvulana [a-wa]: Kijana wa kiume aliyebaleghe na ambaye hajafikia umri wa miaka kama thelathini na tano hivi.

Mfano katika sentensi: Kijana huyo anafanya vibaya, hatii wazaai wake. Amesahau kuwa asiyefunzwa na mamaye hufunzwa na ulimwengu.

 

8. Soko – chete, gulio.

Soko [li-ya]: mahali penye mkusanyiko wa wauzaji na wanunuzi wengi wa bidhaa za rejareja. 

Mfano katika sentensi: Binti na Shaja wametumwa gulioni.

 

9. Nyumbani – kiamboni, mastakimuni, chengoni

Nyumbani [ki]: mahali mtu anakoishi.

Mfano katika sentensi: Nyumbani kwao kuna matunda mengi sana.

 

10. Hasira – mafutu, kero, hamaki, ghadhabu.

Hasira [i-zi]: Ghadhabu.

Mfano katika sentensi: Baba alishikwa na hasira alipoona ngo'mbe wanaharibu mahindi shambani. 

 

11. Lengo – dhamira, nia, azma, kusudi, gharadhi, tarajio, tumaini, matilaba.

Lengo [li-ya]: Kitu au jambo analotazamia mtu.

Mfano katika sentensi: Lengo la Salasha kuu la kwenda gulioni lilikuwa ni kununua mbaazi. 

 

12. Tajiri – mkwasi, mlalaheri

Tajiri [a-wa]: Aliye aliye na mali nyingi.

Mfano katika sentensi: Tajiri huyo alipoaga, aliwacha pesa taslimu bilioni mia saba kwenye benki.

 

13. Maskini – mlalahoi, fukara, hawinde, mkata, fakiri.

Maskini [a-wa]: Mtu asiyekuwa na pato la kutosha.

Mfano katika sentensi: Rais alitoa fedha taslimu bilioni kumi kujenga miradi ya kupea maskini mapato katika nchi yetu. 

 

14. Pesa – njenje, ngwenje, fedha, hela

Pesa [i-zi]: Sarafu au noti zenye dhamani zilizoidhinishwa rasmi kutumika katika ununuzi na uuzaji.

Mfano katika sentensi: Sina hela hata moja kwenye benki.

 

15. Uzembe – uvivu, ajizi.

Uzembe [u]: Hali ya kufanya mambo bila ya makini.

Mfano katika sentensi: Kila wakati wanafunzi wazembe hawapiti mtihani.

16. Maringo – madaha, madaha

Maringo [-ya]: Mwenendo au tabia ya kujivuna.

Mfano katika sentensi: Nilimwona Bi. Harusi akitembea kwa madaha. 

 

17. Uso – wajihi

Uso [u-zi]: Sehemu ya mbele ya kichwa kuanzia kwenye paji hadi kidevuni. 

Mfano katika sentensi: Niamkapo asubuhi, mimi huosha uso wangu. 

 

18.  Mke – ahali.

Mke [a-wa]: mwanamke aliyeolewa. 

Mfano katika sentensi: Mke wa Ngaira ni mpishi hodari.

 

19. Familia – aila, mlango

Familia [i-zi]: Baba, mama, na wana.

Mfano katika sentensi: Tunapenda wageni katika familia yetu. 

 

20. Barabara – tariki, gurufa, baraste.

Barabara [i-zi]: Njia pana ya magari.

Mfano katika sentensi: Barabara kuu ya kwenda Thika imejaa mlolongo wa magari.

 

21. Ugonjwa – maradhi, ndwele.

Ugonjwa [u-ya]: Kitu kinachosababisha mtu, mmea, au mnyama kuwa na afya mbaya.

Mfano katika sentensi: Nyanya amepona ugonjwa wa kifua kikuu.

 

22. Hongo – rushwa, chai, chirimiri, chauchau, kadhongo, chichiri, mvugulio. 

Hongo [i-zi]: Malipo au zawadi anayotoa mtu ili kupata haki. 

Mfano katika sentensi: Watu wengi walipoteza kazi katika nchi ya Tanzania kwa sababu ya kukubali hongo.

 

23. Mwizi – luja, mkupuzi, pwagu, pwaguzi

Mwizi [a-wa]: Mtu mwenye tabia ya kuchukua kisicho chake bila ruhusa. 

Wezi watatu walishikwa na polisi mafichoni mwao kando ya mto Zambezi.

 

24. Jela – gereza, husuni

Jela [i-zi]: Pahali wanapowekwa wahalifu wa sheria, waadhibiwe ili wajirekebishe.

Mfano katika sentensi: Mati alishangaa kuwaona kina mama gerezani. 

 

25. Afya – siha, udole

Afya [i-zi]: Hali nzuri ya mwili, bila ya magonjwa. 

Mfano katika sentensi: Mimea hiyo ina afya nzuri.

 

26. Jitimai - huzuni, kihoro, simanzi. 

Jitimai [-i]: Hali ya kuwa na masikitiko au majonzi.

27. Fujo – ghasia, zogo, zahama

Fujo [i-zi]: Hali ya kutokuwako utulivu. 

Mfano katika sentensi: Fujo ilizuka wakati wanariadha hawa walipotangazwa washindi.

 

28. Ukuta – kiambaza

Ukuta [u-zi]: Sehemu ya nyumba kutoka chini iliyosimama wima.

Mfano katika sentensi: Ukuta ule una nyufa.

 

29. Usingizi – ndezi, gonezi,

Usingizi [-u]: Hali ya kupumzika kwa mwili na akili wakati wa kulala.

Mfano katika sentensi: Niliota nikiwa usingizini.

 

30. Kazi – amali, gange

Kazi [i-zi]: shughuli anayofanya mtu.

Mfano katika sentensi: Kazi yake ni kutumwa ofisini.

 

31. Mavazi – lebasi

Mavazi [li-ya]: kitu kama vile nguo, au ngozi, kinachovaliwa mwilini.

Mfano katika sentensi: Wana hawa watavaa mavazi meupe.

 

32. Mtoto – mkembe

Mtoto [a-wa]: Mwana mchanga

Mfano katika sentensi: Mtoto huyu ana vidonda kwenye miguu yake. 

 

33. Makamu – naibu

Makamu [a-wa]: Mtu wa pili katika cheo.

Mfano katika sentensi: Makamu wa rais ana kesi kortini.

 

34. Kitanda - Samadari

Kitanda [ki-vi]: kifaa cha nyumbani chenye umbo wa mstatili na miguu minne, kinachotumiwa kwa kulalia. 

Mfano katika sentensi: Kitanda ulichokilialia hujui kunguni wake.

35. Moyo – mtima,  fuadi.

Moyo [u-i]: kiungo cha mwili kilichoko kwenye sehemu ya kifua kati ya mapafu, ambacho husukuma damu ili ienee mwilini kwa kupitia kwenye mishipa. 

Mfano katika sentensi: Babu alipatikana na ugonjwa wa msukumo wa damu.

 

36. Kijiji – kitongoji, kaya, karia.

Kijiji [ki-vi]: mahali panapoishi watu wengi pamoja ambapo si mji.

Mfano katika sentensi: Kwetu kiamboni kumejaa nyani. 

 

37. Fanicha – samani

Fanicha [i-zi]: vyombo vya nyumbani kama vile meza, viti, vitanda, na kabati.

Mfano katika sentensi: Mama yangu anatengenezewa fanicha zake kwenye karakana ya Bwana Mcheshi.

 

38. Ndoa – nikahi, nikaha, arusi.

Ndoa [i-zi]: Makubaliano rasmi ya mwanamume na mwanamke kuishi pamoja kama mume na mke.

Mfano katika sentensi: Bwana na Bi. Martin wanatia sahihi cheti chao cha ndoa.

 

39. Ndoto – ruiya, njozi. 

Ndoto [i-zi]: maono yatokeayo usingizini. 

Mfano katika sentensi: Maina aliota ndoto kwamba amesafiri na malaika. 

 

40. Soka - kandanda, gozi, kabumbu.

Soka [i-zi]: mchezo wa mpira wa miguu.

Mfano katika sentensi: Kijana huyu anapenda sana kucheza soka.

 

41. Furaha – faraja, bashasha, naima, ucheshi

Furaha [i]: Hali ya uchangamfu, au ukunjufu wa moyo. Pia yaweza kumaanisha hali ya kuridhika.

Mfano katika sentensi: Nilijawa bashasha, nilipomwona mwanangu aliyepotea amerejea mastakimuni. 



  • banati by Midas touch used under CC_BY-SA
  • nyumbani by Home Dzine used under CC_BY-SA
  • rafiki by Global giving used under CC_BY-SA
  • soko by move bubble used under CC_BY-SA
  • waya by pinterest used under CC_BY-SA
  • malaika by eLimu used under CC_BY-SA
  • nina by Elimu used under CC_BY-SA
  • furaha by Public enemy Africa used under CC_BY-SA
  • maskini by eLimu used under CC_BY-SA
  • moyo_1 by Various sources used under CC_BY-SA
  • mtoto by pinterest used under CC_BY-SA
  • mvivu by dreamstime used under CC_BY-SA
  • pesa by pinterest used under CC_BY-SA
  • aila by eLimu used under CC_BY-SA
  • bara by Tuko.co.ke used under CC_BY-SA
  • jela by eLimu used under CC_BY-SA
  • kipusa2 by Midas touch used under CC_BY-SA
  • kitanda by bfd used under CC_BY-SA
  • Harusi by Spirit of black Paris used under CC_BY-SA
  • kijiji by Joke used under CC_BY-SA
  • moyo by Various sources used under CC_BY-SA
  • samani by eLimu used under CC_BY-SA

  • Creative Commons License
    All work unless implicitly stated is licensed under a Creative Commons Attribution-NonCommercial-NoDerivatives 4.0 International License.